Wednesday 18 February 2015

MTOTO ALBINO YOHANA BAHATI AUWAWA SHILABELA




Mwili wa mtoto Yohana Bahati aliyekuwa na umri wa mwaka mmoja ambaye ni mlemavu wa ngozi maarufu kama Albino, alitekwa siku ya Jumapili February 15, 2015 amepatikana ameuawa katika eneo la Shilabela Mapinduzi kilomita kadhaa kutoka nyumbani kwao kijiji cha Ilelema .Polisi wanaeleza kuwa waliukuta mwili huo katika msitu wa hifadhi wa Biharamulo leo majira ya alfajiri akiwa amekatwa mikono na miguu yake.
Wakati mwili wa mtoto Yohana ukipatikana ,mama wa mtoto huyo bi , Ester Jonas mwenye umri wa miaka 30 bado hali ya afya yake ni tete na amelazwa katika hospitali ya rufaa ya Bugando , Mwanza . Madaktari walimfanyia upasuaji mwanamke huyo aliyekuwa amekatwa kwa panga usoni mwake na sehemu zingine za mwili majeraha ambayo aliyapata wakati alipokuwa akijaribu kumuokoa mwanawe, Yohana kutoka mikononi mwa wauaji .
Dada zake Yohana Tabu bahati mwenye umri wa miaka mitatu bado yuko mikononi mwa uangalizi wa askari polisi. Dada yao mkubwa ambaye pia ni Albino Shida Bahati mwenye umri wa miaka kumi na miwili amehamishwa kijijini hapo tangu tukio hilo litokee, na anatunzwa na jamaa zake katika kijiji jirani.
Mpaka sasa watu wengine wawili zaidi wamekamatwa na polisi wakihusishwa na tukio hilo ingawa baba mzazi wa mtoto huyo, bado anashikiliwa na polisi.
Mwezi uliopita serikali ya Tanzania ilipiga marufuku waganga wa kienyeji pia kupiga marufuku wapiga ramli wote ambao wanaelezwa kuchangia mauaji ya watu hao wenye ulemavu wa ngozi.. waganga wa kienyeji wanaamini kwamba viungo vya mwili wa Albino huleta bahati na utajiri kwa anaye vipata.katazo hilo ni sehemu ya mkakati maalumu wa kupunguza kama sio kuondosha kabisa mashambulizi ya watu wenye ulemavu wa ngozi.

No comments:

Post a Comment